Sunday, September 8

Mashahidi waingia mitini Pemba, wasababisha kesi ya ubakaji kuondolewa

IMEANDIKWA NA ZUHURA JUMA, PEMBA

Mahakama ya Mkoa Wete imeiondoa kesi namba 75 ya mwaka 2019 iliyokua inamkabili kijana Khamis Abdalla Khamis mwenye miaka 35 aliyetuhumiwa kumbaka mtoto mwenye umri wa miaka kumi baada ya mashahidi kutofika Mahakamani.

Akitoa uamuzi huo Mrajisi wa Mahakama kuu Pemba Abdul-razak Abdul-kadir Ali amesema, analiondosha shauri hilo chini ya kifungu cha 103 (9) cha sheria nambari 7 ya mwaka 2018.

“Kifungu hiki kinanipa uwezo wa kuliondosha shauri ikiwa mashahihdi wameshindwa kufika mahakamani”, alisema Mrajis huyo.

Alisema kuwa, upande wa mashitaka unaweza kulifungua tena shauri hilo iwapo watawapata mashahidi na na kuwapeleka mahakamani.

“Upande wa mashitaka mtakapopata mashahidi wa kesi hii basi mnaweza kulirudisha tena lakini kwa leo nimeliondosha”, alifafanua.
Kesi hiyo ilianzwa kusikilizwa kwa mara ya kwanza Oktoba 1, mwaka jana katika mahakama ya mkoa Wete.
Ilidaiwa Mahakamani hapo na Mwendesha Mashitaka kutoka ofisi ya Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) Juma Mussa Omar kuwa mtuhumiwa anatuhumiwa kutenda makosa mawili.

Ambapo kosa la alilitenda baina ya Septemba 01 na Septemba 20 mwaka jana saa zisizofahamika katika maeneo ya Konde Wilaya ya Micheweni Mkoa wa Kaskazini Pemba mtuhumiwa huyo alimbaka mtoto mwenye umri wa miaka kumi, jambo ambalo ni kosa kisheria.

Kufanya hivyo ni kosa kisheria kinyume na kifungu cha 108 (1) (2) (e) na 109 (1) cha Sheria ya adhabu namba 6 ya mwaka 2018 sheria ya Zanzibar.

Kosa la pili kwa mshitaka ilidaiwa kulitenda siku hiyo hiyo mwaka jana saa zisizofahamika Konde alimuingilia kinyume na maumbile mtoto huyo jambo ambalo ni kosa kisheria.

Kufanya hivyo ni kosa kisheria kinyume na kifungu cha kifungu cha 115 cha sheria namba 6 ya mwaka 2018.