Friday, October 18

Wajumbe wa kamati washauriwa.

WAJUMBE wa kamati za mashauriano za shehia kutoka Wilaya nne za Pemba, zimeombwa kuwa makini na kujifunza mambo mazuri kutoka katika kamati ambazo zimekua za mfano.

Wajumbe wa kamati hizo wamekutana hivi karibuni, katika skuli ya msuka Sekondari Wilaya ya Micheweni kwa lengo la kuwasilisha mipango kazi yao ambayo wameitekeleza katika shehia zao na kutoa mafanikio.

Akizungumza na waandishi wa habari Afisa Miradi kutoka Taasisi ya Milele Zanzibar Foundation, Fatma Khamis Silima alisema mashirikiano ni jambo zuri kwa viongozi wakamati hizo, katika kusaidiana pale ambapo kamati moja inapohitaji kujifunza kwa wenzake.

Alisema zipo kamati zimefanya vizuri katika utekelezaji wa mipango kazi yake, ni vyema kwa kamati nyengine kujifunza huko ili kamati zote kuwa na mipango kazi bora.

“Suala la kutengeneza mipango kazi na kuibua changamoto ni suala la kamati husika, vizuri leo tumekutana hapa wajumbe kutoka kamati 12 za shehia ambazo zimepewa elimu, na hizi kamati saba tutazifikia haraka”alisema.

Naye afisa miradi ya afya kutoka Taasisi ya Milele Shakira Hasnu, alisema mambo yanayopatikana msuka yanapaswa kuingwa na kamati nyengine za shehia.

Mjumbe kutoka kamati ya mashauriano ya Mtambwe Kusini Khamis Khalfan Khami, alisema katika shehia yao wameweza kuwashajihisha wanafunzi kupenda kusoma masomo ya sayansi na wameweza kuhamasika, ili kuweza kusaidia jamii zao hapo baadae.

“Kwa muda mrefu katika maeneo yetu ya visiwani tumekuwa na taatizo la madaktari, tumeweza kushajihisha wanafunzi kusoma masomo hayo, ili kuja kusaidia familia zao zilizoko katika visiwa”alisema.

Mjumbe kutoka Makati ya Msuka Mashariki Abdalla Hamad Shehe, alisema kamati hiyo imeweza kutoa mafunzo kwa vijana 280 kujifunza vitu mbali mbali vya ujasiriamlia, ikiwemo suala zima la kilimo, ufugaji, ili vijana kutokuwa na muda wa kukaa vibarazani.

Alisema waliweza kushirikiana na wazazi katika kuwarudisha watoto waliotoroka skuli, pamoja na kuweka mikakati mizito kwa wazazi watakao shinda kuwashajihisha watoto kusoma na kuwaachia kwenda baharini.

Kwa upande wake Tatu Daudi Ali kutoka shehia ya Michezani, alisema Milele imeweza kupunguza tatizo la msongamano wa mama wajawazito pamoja na akina mama kuhamasika kuwapatia chanjo watoto wao.