Saturday, October 19

Wapongeza kasi ya DK. Mwinyi.

 

WANANCHI na Viongozi wa Serikali Kisiwani Pemba, wamepongeza Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa baraza la Mapinduzi Dk Hussein Ali Mwinyi, kwa kasi alioanza nayo katika kuingoza Zanzibar katika kipindi cha miaka mitano.

Walisema kutokana na kasi aliyoanza nayo kwa kuteuwa viongozi vijana, akiwemo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Hemed Suleiman Abdalla, pamoja na kunza kwa ziara yake ya kwanza bandarini ni dhahiri kuwa awamu yake itakuwa ni uchapaji wa kazi kwa vitendo.

Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa nyakati tafauti, Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Pemba Omar Khamis Othaman alisema kwa kasi aliyoanza nayo DK.Mwinyi ni yakupongezwa, hivyo viongozi na wananchi kujipanga kwendana na kasi yake.

Alisema vijana wanapaswa kumuunga mkono Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa baraza la Mapinduzi Dk.Mwinyi, ili kufikia malengo na dhamira zake alizoziweka.

“Sisi viongozi tunapaswa kujipanga kwa kina ili tuweze kwendana na kasi yake, katika awamu hii kila mtu anapaswa kuwa makini na kuhakikisha anachokifanya anakifanya kwa umakini mkubwa”alisema.

Akizungumzia suala la uchaguzi, alisema kwa sasa uchaguzi umekwisha kilichobakia ni utendaji wa kazi na uwajibikaji na sio siasa tena.

Hata hivyo aliwataka vijana kuachana na tabia ya kukaa vibarazani na kuhubiri siasa, sasa sio wakati wake tena bali ni wakati wa kwenda sambamba na kasi ya Dk.Miwnyi katika kuhimiza maendeleo.

Kwa upande wa suala la amani na utulivu, aliwahimiza vijana, wazazi na wazee kuhakikisha wanaiendelezeza amanai iliyopo na inadumu kwa muda mrefu.

Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Kusini Pemba Yussuf Juma Ali, alisema  kasi kasi aliyoanaza nayo Dk.Mwinyi ni yakupongezwa katika uongozi, huku akimtaka kuendelea na kasi hiyo ya kuitekeleza kwa vitendo Ilani ya CCM 2020/2025.

Alisema kutokana na kasi hiyo viongozi atakaowateuwa, hawanabudi kuendana na kasi ya Rais katika suala la kuwapelekea maendeleokwa wananchi.

Afisa Mdhamini Wizara ya Vijana Utamadunia Sanaa na Michezo Pemba, Fatma Hamad Rajib alipongeza Dk Mwinyi kwa kuchaguliwa kwake kuongoza Zanzibar, sambamba kasi ya utendaji wake aliyoanza nayo.

Kwa upande wao Vijana wamesema wameanza kujenga matumaini makubwa na uongozi wa Serikali ya awamu ya nane, chini ya Dk.Hussein Mwinyi na Makamu wake wa pili wa Rais.

Hashil Fadhil Abdulla alisema vijana wapo tayari kwenda na kasi aliyoanza nayo Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa baraza la Mapinduzi, katika uongozi wake kwa kuhakikisha wanachapa kazi ipasavyo.

Hata hivyo aliwataka watendaji watakaoteuliwa kuwatupia macho Vijana, kwani ndio tegemeo la taifa la baadae na ndio nguvu kazi ya Taifa.