Friday, October 18

WATAKIWA KUJITOKEZA KUUNGA MKONO WATU WENYE ULEMAVU

AFISA Mdhamini Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Pemba Ahmed Abuubakar Mohd, akitoa taarifa kwa waandishi wa habari Kisiwani Pemba, juu ya uwepo wa SMILE PEMBA MARATHON, yenye lengo la kusaidia vifaa kwa watu wenye ulemavu, mkutano uliofanyika mjini Chake Chake

NA ABDI SULEIMAN.

MAKAMU wa Pili wa Rais Zanzibar Hemed Suleiman Abdulla, anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika mbio za smile pemba marathon(spm) zinazotarajiwa kufanyika Mwezi Dimbemba mwaka huu Kisiwani Pemba.

Akitoa taarifa kwa waandishi wa habari Kisiwani Pemba, juu ya uwepo wa mbio hizo ambazo tayari maandalizi yake yameshaanza, afisa mdhamini Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais Ahmed Abuubakar Mohd, alisema lengo kubwa la mbio hizo ni kupata vifaa tiba, vifaa kazi kwa kuweza kuwasaidia watu wenye ulamavu.

Alisema kwa mujibu wa sense ya Taifa 2020/2022, kwa upande wa Pemba kuna watu wenye ulamavu 3000, ambapo kwa kwenye mbio hizo wanaweza kuwasaidia watu 1000, katika kuhakikisha wanapatiwa vifaa tiba na saidizi, ili kupunguza au kuondoa changamoto kwa wale ambao watabahatika kupatiwa.

Aidha alifahamisha kwamba mbio hizo zinatarajiwa, kufanyika katika wiki ya kuadhimisha siku ya watu wenye ulamavu duniani ambayo hufanyika Disemba 3 kila mwaka.

“Katika wiki hiyo sisi Pemba tutakua na harakati mbali mbali, ila tutahakikisha tunakusanya vifaa tiba, vifaa saidizi, ili kuweza kufurahi na watu wenye ulemavu kivitendo na jamii nayo inashiriki katika mazoezi kikamilifu,”alisema.

wajumbe wa kamati ya marathoni Kisiwani Pemba

Katika hatua nyengine, Mdhamini Ahmed alisema lengo na madhumuni ya marathoni hiyo, ni kushajihisha na kuwaweka pamoja watu wenye ulemavu na walemavu watarajiwa, pamoja na kutia nguvu harakati za kuwasaidia katika kupata mahitaji na maslahi yao ya kila siku.

Hata hivyo alisema mbio hizo zimegawika katika makundi mbali mbali Mita 100 kwa wanaoendesha baskeli za watu wenye ulamvu, KM 5, KM 10, KM 21, mbio hizo zitazunguruka mji mzima wa chake chake ili kuwapa nafasi wananchi wote kushirikia.

Aliwataka wananchi na watanzania kuhakikisha wanajitokeza katika kushiriki mbio hizo, ili kuhakikisha jina lililoibunia linasibu katika mbio hizo la smile pemba marathon.

Alisema katika mbio hizo bado wanakaribisha wadau kutoka makampuni mbali mbali, ili kuona malengo ya kupatiwa vifaa tiba watu wenye ulemavu vinapatikana.

baadhi ya wajumbe wa kamati ya marathoni Kisiwani Pemba

“Mwisho wa siku watu wenye ulemavu, tunahakikisha wanaoishi ndani ya Kisiwa cha Pemba na maeneo jirani, basi wanapatiwa misaada itakayopatikana kupitia mbio hizo za marathoni,”aliserma.

Nae Meneja wa TTC Pemba Khamis Salum Ali, alisema TTC imeguswa kwa ajili ya kuwasaidia watu wenye ulemavu kuwapatia vifaa pamoja na kuunga mkono juhudi za SMT na SMZ katika kuona watu wenye ulemavu wanufaika na matunda ya serikali yao.

Kwa upande wake Meneja wa TRA Mkoa Kikanda Arif Mohamed Said, alisema wameona ni bora kuwaunga mkono watu wenye ulamavu na kuona wako sawa kama watu wasio na ulemavu.

MWISHO

Abdi Juma Suleiman

Journalist/Photographer

Zanzibarleo newspaper/habari portal/ blog
Chake Chake -Pemba
+255774565947 or +255718968355