Saturday, October 19

UNESCO yakutana na walimu.

MKUFUNZI Hasina Bukheti kutoka shirika la Umoja wa Mataifa Elimu Sayansi na Utamaduni (UNESCO)akiwasilisha mada wakati wa mafunzi ya stadi za maisha, Ukimwi, Afya ya uzazi na elimu ya jinsia, kwa walimu wa skuli za Sekondari na Msingi Wilaya ya Mkoani, huko katika skuli ya Mohamed Juma Pindua Mkanyageni.(PICHA NA ABDI SULEIMAN, PEMBA)

SHIKIKA la Umoja wa Mataifa elimu Sayansi na Utamaduni (UNESCO) limewata walimu wa skuli za sekondari na msingi Wilaya ya Mkoani, kuyatumia vyema mafunzo ya stadi za maisha, Ukimwi, afya ya uzazi na elimu ya jinsia, ili kuweza kuwasaidia wanafunzi wao katika kufikia malengo yao ya kielimu.

Hayo yameelezwa na mratibu wa miradi kutoka shirika la UNESCO Dar Esaalam Viola Muhangi, wakati alipokuwa akizungumza na walimu hao, kabla ya kuanza kwa mafunzo ya siku sita huko katika skuli ya Mohamed Juma Pindua Mkanyageni Wilaya ya Mkoani.

Alisema mafunzo hayo ya ni muhimu sana kwa walimu katika kuwasaidia wanafunzi wao kuweza kufikia malengo yao ya kielimu, kwani wananfunzi wengi wamekuwa wakikatisha ndoto zao mapema.

Alifahamisha kuwa wilaya ya mkoni ndio wilaya ya kwanza kwa Zanzibar kunufaika na mafunzo hayo, kwenye wilaya nne za Tanzania hivyo walimu wanakila sababu ya kujifunza mbinu mbali za kuwasaida wanafunzi.

“Nyinyi walimu muna bahati sana kwetu, mumekuwa ni Wilaya ya kwanza kunufaika na mafunzo haya, katika wilaya nne za Tanzania hii ni fursa pekee kwenu katika kufikia malengo ya kuwasaidia wanafunzi”alisema.

Aidha aliwashukuru walimu hao kwa ushiriki wao kikamilifu, kwani mafunzo hayo yataweza kuwajengea uwezo walimu katika kuongeza ujuzi katika masuala ya afya ya uzazi.

 

Akifungua mafunzo hayo kwa niaba ya Afisa Mdhamini Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Pemba, afisa Elimu Sekondari Mwalimu Haji amesema wilaya ya mkoani ni lulupekee kuwa ya kwanza katika wilaya nne za Tanzania kupatiwa mafunzo hayo.

Aliwataka walimu hao kuhakikisha elimu hiyo wanaifikisha kwa walimu wenzao na wanafunzi wao, ili vijana wanaowasimamia maskulini kuweza kufikia malengo yao.

Aidha aliwasisitiza walimu hao kuwa makini katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi, kujiepusha na vibaraza baraza pamoja na mambo yasio na tija kwao.

Naye mkuu afya ya uzazi kutoka shirika la UNESCO Tanzania Mathias Herman, alisema sera ya elimu imeeleza mambo mbali mbali hivyo utoaji wa mafunzo hayo ya juu ya stadi za maisha, elimu ya jinsia, afya ya uzazi na ukimwi ni miongoni mwa mikakati ya sera hiyo.

Alisema katika miaka ya hivi karibuni wanafunzi wamekuwa wakikumbana na changamoto nyingi, ikiwemo unyanyasaji wa kijinsia, kujiingiza katika mauhusiano yanayopelekea kupata mimba na kupelekea kukatisha masomo yao.

“Mradi huu utawajengea uwelewa walimu wa skuli za msingi na sekondari, katika masuala ya afya ya uzazi, stadi za maisha ili kuwaelimisha wanafunzi wao na kukabiliana na changamoto za vishawishi”alisema.

Kwa upande wake afisa kutoka UNESCO Hasina Bukhet, alisema katika kiipindi cha hivi karibuni matukio ya ubakaji, watoto kujiingiza katika masuala ya ushoga, ulawiti ambapo waathirika wakubwa ni wanafunzi wa matukio hayo.

Alisema matukio hayo yamekuwa yakikatisha hata ndoto na malengo ya vijana katika elimu, kwani kwani wengi wao wanalazimika kubaki majumbani kutokana na kuona aibu.

Afisa kutoka kitengo cha ushauri nasaha kutoka wizara ya elimu Wlimu Zanzibar Halima Ahmada, alisema matuko ya udhalilishaji yamekuwa yakikatisha ndoto za wanafunzi, kwani kesi zilizoripotiwa wizarani ni kidogo sana kuliko zilizokuwa hazijaripotiwa.

Kwa upande wao Fatma Hashim na Dk.Abdalla omar kutoka Kitengo shirikishi Pemba, wamewataka walimu hao kuwa wawazi wanapozungumzia masuala ya afya ya uzazi, ili vijana kuendelea kuchukua tahadhari wakati wakiwa maskulini.